MASOMO YA MISA ,JUMATANO,20 SEPTEMBA,2023

MASOMO YA MISA JUMATANO

SOMO 1

1Tim 3:14-16
Nakuandikia hayo, nikitaraji kuja kwako hivi karibu. Lakini nikikawia, upate kujua jinsi iwapasavyo watu kuenenda katika nyumba Mungu, iliyo kanisa la Mungu aliye hai, nguzo na msingi wa kweli. Na bila shaka siri ya utauwa ni kuu: Mungu alidhihirishwa katika mwili, Akajulika kuwa na haki katika roho, Akaonekana na malaika, Akahubiriwa katika mataifa, Akaaminiwa katika ulimwengu, Akachukuliwa juu katika utukufu.

Wimbo wa Katikati
Zab 111: 1-6

Nitamshukuru Bwana kwa moyo wangu wote,
Barazani pa wanyofu wa moyo na katika mkutano.
Matendo ya Bwana ni makuu.
Yafikiriwa sana na wapendezwao nayo. 
(K) Matendo ya Bwana ni makuu. 

Kazi yake ni heshima na adhama,
Na haki yake yakaa milele.
Amefanya ukumbusho wa matendo yake ya ajabu;
Bwana ni mwenye fadhili na rehema. 
(K) Matendo ya Bwana ni makuu. 

Amewapa wamchao chakula;
Atalikumbuka agano lake milele.
Amewajulisha watu wake uwezo wa matendo yake,
Kwa kuwapa urithi wa mataifa. 
(K) Matendo ya Bwana ni makuu.

Shangilio
Lk 6:63,68

Aleluya, aleluya,
Maneno yako, Bwana, ni roho na uzima. Wewe unayo maneno ya uzima wa milele.
Aleluya.

INJILI
Lk 7:31-35
Wakati ule: Jesu aliwaambia makutano, "Niwafananishe na nini watu wa kizazi hiki, nao wamefanana na nini? Wamefanana na watoto walioketi sokoni na kuitana, wakisema, 'Tuliwapigia filimbi wala hamkucheza; tuliomboleza, wala hamkulia.'Kwa kuwa Johane Mbatizaji alikuja, hali mkate wala hanywi divai, nanyi mwasema, 'Ana pepo.' Mwana wa Adamu amekuja, anakula na kunywa, nanyi mwasema, 'Tazama, mlafi huyu, na mnywaji wa divai, rafiki wao watoza ushuru na wenye dhambi.' Na hekima imejulikana kuwa ina haki kwa watoto wake wote."

No comments

Post a Comment

Shajara Yetu © all rights reserved
MKATOIKI KIGANJANI by mitume technologies