MTAKATIFU WA LEO 13JUNI | Mt. Antoni wa Padua, Padre na Mwalimu wa Kanisa

Kumbukumbu ya Mtakatifu Anthoni wa Padua Padre na Mwalimu wa Kanisa

Kanisa kila mwaka ifikapo tarehe 13 Juni, linaadhimisha Kumbukumbu ya Mtakatifu Anthoni wa Padua, Padre na Mwalimu wa Kanisa: mhubiri mahiri wa Injili ya Kristo iliyomwilishwa katika huduma makini kwa maskini na wale wote waliokuwa wanasukumizwa pembezoni mwa jamii. Huu ni mwaliko kwa waamini kujenga utamaduni wa kusoma, kulitafakari na hatimaye, kulimwilisha Neno la Mungu katika uhalisia wa maisha yao. Kumfahamu Kristo kwa Njia ya Neno!

Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S. – Vatican.

Baba Mtakatifu Francisko mara baada ya Katekesi yake Jumatano tarehe 12 Juni 2024 kuhusu: “Roho Mtakatifu na Bibi Arusi. Roho Mtakatifu anawaongoza watu wa Mungu kuelekea kwa Yesu, tumaini letu” amesema, Kanisa kila mwaka ifikapo tarehe 13 Juni, linaadhimisha Kumbukumbu ya Mtakatifu Anthoni wa Padua, Padre na Mwalimu wa Kanisa: mhubiri mahiri wa Injili ya Kristo iliyomwilishwa katika huduma makini kwa maskini na wale wote waliokuwa wanasukumizwa pembezoni mwa jamii. Huu ni mwaliko kwa waamini kujenga utamaduni wa kusoma, kulitafakari na hatimaye, kulimwilisha Neno la Mungu katika uhalisia wa maisha yao. Kwa njia ya Neno la Mungu, Kristo Yesu anang’arisha na kupyaisha maisha ya waja wake. Na hii ni njia pia ya kumfahamu Kristo Yesu aliyeteswa, akafa na kufufuka kwa wafu utimilifu wa Ufunuo wa Neno la Mungu, tayari kumtangaza na kumshuhudia. Hii ni changamoto kwa waamini kuwa kweli ni chumvi ya dunia na mwanga wa Mataifa kwa kumsifu na kumtukuza Mwenyezi Mungu kwa njia ya ushuhuda wa maisha yenye mvuto na mashiko. Huu ni mwaliko kwa waamini pamoja na watu wote wenye mapenzi mema kujiachilia na kujiaminisha kwa Roho Mtakatifu na kamwe wasitafute njia za mkato katika maisha ya kiroho! Waamini wanaswa kuwa ni chumvi ya dunia na mwanga wa mataifa, mambo msingi katika mchakato wa uinjilishaji mpya unaofumbatwa katika ushuhuda makini kwa Kristo na Kanisa lake, kazi inayotekelezwa kwa ufanisi mkubwa na Roho Mtakatifu.

Ushuhuda wa waamini unamtolea Mwenyezi Mungu sifa na utukufu, utimilifu wa changamoto za Kiinjili zilizotolewa na Kristo Yesu katika maisha na utume wake hapa duniani. Daima, Kristo Yesu alijitahidi kutekeleza mapenzi ya Baba yake wa mbinguni hapa duniani, akamtuma Roho wake Mtakatifu, ili aweze kuwapaka mafuta waja wake, tayari kwenda sehemu mbalimbali za dunia kutangaza na kushuhudia utukufu, ukuu na uweza Mungu katika maisha ya mwanadamu. Waamini wajitahidi kushuhudia mwanga uliomo ndani mwao, ili kumtukuza Baba yao wa mbinguni. Wawe ni chumvi inayokoleza utakatifu wa maisha, ili kufukuzilia mbali rushwa na ufisadi; mambo yanayowanyanyasa watu duniani. Waamini wajitahidi kuwa ni vyombo na mashuhuda wa ukweli kwa kusema “Ndiyo” na “Ndiyo” yao iwe imekamilika pasi na mawaa, kinyume cha hapo, kuna hila za Shetani. Baba Mtakatifu anakaza kusema, Kristo Yesu ameliaminisha Kanisa lake kuwa ni chombo na shuhuda wa usalama na ukweli, kama zawadi kutoka kwa Mwenyezi Mungu; zawadi inayopaswa kumwilishwa katika uhalisia wa maisha ya watu! Ushuhuda usaidie kuyatakatifuza malimwengu, ili watu waweze kutembea katika mwanga wa maisha mapya. Waamini wasipokuwa makini, ushuhuda wao utakosa mvuto, dira na mwelekeo sahihi katika maisha na hizi ni dalili za kutokubali kumpokea Kristo Yesu na Roho wake Mtakatifu.

Mtakatifu Antoni wa Padua alifariki dunia 13 Juni 1231

Itakumbukwa kwamba, Mtakatifu Anthoni wa Padua alizaliwa tarehe 15 Agosti 1195 huko Lisbon nchini Ureno. Katika umri wa ujana wake, alijisadaka sana kutangaza na kushuhudia Habari Njema ya Wokovu. Mtakatifu Anthoni wa Padua alikuwa ni mtu wa sala na tafakari ya kina katika maisha yake, kiasi cha kuwavuta watu wengi kufanya toba na wongofu wa ndani. Alifariki dunia tarehe 13 Juni 1231, huko Arcella, Padua, Italia, akiwa na umri wa miaka 35 tu, matendo makuu ya Mungu. Papa Gregori wa IX, hapo tarehe 30 Mei 1232, akiwa mjini Spoleto, Italia, akamtangaza kuwa Mtakatifu. Tarehe 16 Januari 1246 Papa Pio XII akamtangaza kuwa Mwalimu wa Kanisa “Doctor Evangelicus” yaani “Mwalimu wa Injili”. Hii ni kutokana na amana na utajiri uliokuwa unabubujika kutoka katika mahubiri yake yaliyokuwa yanapata chimbuko lake katika Injili. Ibada kwa Mtakatifu Anthony wa Padua imeenea sehemu nyingi za dunia.

No comments

Post a Comment

Shajara Yetu © all rights reserved
MKATOIKI KIGANJANI by mitume technologies